MKUU wa Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro, Herman Kapufi, amekiri kuwa
Halmashauri ya Wilaya hiyo imezidiwa nguvu na wazazi ambao
wanashirikiana na watuhumiwa wanaowapa mimba Wanafunzi ambao
hawajamaliza masomo katika shule za Msingi na Sekondari Wilayani humo.
Kapufi ameyasema hayo wakati akiongea katika mazungumzo maalumu na waandishi wa habari,
ambapo alidai jambo linaloisumbua Wilaya hiyo ni pamoja na watoto
kukeketwa katika umri mdogo wakati Halmashauri ya Wilaya ikiwa inafanya
juhudi za kuwakamata wanaoshiriki vitendo hivyo.
Hata hivyo alisema, katika kipindi cha mwaka jana takribani wanawake 37
wamekamatwa na Jeshi la Polisi katika eneo la Kavambughu wilayani humo
wakiwa wanawakeketa watoto wachanga ambapo wamefikishwa mahakamani
kujibu tuhuma dhidi yao (kesi bado inaendelea).
“Sheria za Nchi zinasema Msichana asiolewe akiwa na umri chini ya miaka
kumi na nane awe anasoma au hasomi na kimsingi na wale wanaowakeketa
wakiwa wadogo kabla hawajakomaa ili tusigundue bado tunaendelea kufanya
uchunguzi ili kuwafikisha katika vyombo vya dola” alisema Kapufi
Takwimu zinaonyesha Wilaya ya Same imekuwa kinara wa kukeketa watoto
wachanga na hivyo tatizo hilo kuwa sugu katika Wilaya hiyo.
Afisa Utawala wa Shirika lisilo la kiserikali linalojihusisha na
maendeleo ya mwanawake Afya na Haki za Binadamu (LUDEF), Janeth Malibwi, alisema bado mila za ukeketaji katika
Wilaya hiyo zinaendelea na kwamba kwa sasa wanakeketa watoto wachanga
(pindi wanapozaliwa), jambo ambalo ni hatari kwa Afya zao
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni