Wanawake wameaswa kutumia fursa
iliyopo katika sekta ya bahari kwa kupata elimu na mafunzo ya sekta hiyo
ambayo ni msingi wao katika kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia
ukuaji sayansi na teknolojia inayoongezeka kwa kasi duniani.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa
Usalama wa Mazingira Majini Tumpe Mwaijande kutoka Wizara ya Uchukuzi
kwaniaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Shaaban Mwinjaka wakati wa
ufunguzi wa mkutano wa mwaka wa Umoja wanawake walio katika Sekta ya
masuala ya Bahari Mashariki na Kusini mwa Afrika (WOMESA) ulifanyika jana Dar es salaam.
![]() |
| Mwenyekiti wa WOMASA kutoka Mauritius Bi. Meenaksi Bhirugnath Bhookun akitoa mada wakati wa ufunguzi wa mkutano huo |
Katika mkutano huo wa siku nne
ambao umeanza leo oktoba 28 na unatarajiwa kumalizika Oktoba 31 mwaka
huu, mada mbalimbali zitajadiliwa ikiwemo mpango mkakati wa WOMESA
kuhusu ushiriki wa wanawake katika masuala ya sekta ya bahari katika
nchi wanachama.
Kwa upande wake Mkurugenzi
Msaidizi kutoka Shirika la Kimataifa linaloshughulikia Mambo ya Bahari
(IMO) Pamela Tansey amesema kuwa WOMESA imekuwa msatari wa mbele katika
kumwendeleza mwanamke kwenye sekta ya bahari.
Pamela amesisitiza kuwa wajumbe
wa mkutano huo ni vema waelewe na kusimamia dira ya WOMESA ambayo lengo
lake ni kuwawezesha wanawake kupata ajira katika sekta ya masuala ya
bahari kwa njia ya kupta elimu na mafunzo katika kuendeleza taaluma yao
juu ya masuala ya bahari.
Mkutano huo wa WOMESA
unajumuisha wajumbe 52 kutoka nchi mbalimbali wanachama zikiwamo
Ethiopia, Namibia, Komoro, Visiwa vya Shelisheli, Zambia, Mauritius na
Kenya.
Nchi nyingine ni Angola, Sudani,
Lesotho, Uganda, Somalia, Eritrea, Botswana, Rwanda, Madagaska, Afrika
Kusini, Msumbiji, Burundi, Malawi, Djibout, Zimbabwe na wenyeji
Tanzania.
Mkatano huo wa siku nne
unafanyika nchini chini ya ufadhili wa Mamlaka ya Bandari Tanzania
(TPA), Taasisi ya Masuala ya Bahari Tanzania (DMI), shirika la mfuko
wa hifadhi ya jamii (NSSF) kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa
linaloshughulikia Mambo ya Bahari (IMO) na Shirika la Kimataifa la
Maendeleo (UNDP).


Hakuna maoni:
Chapisha Maoni